Fransia Mwakapalila (wa kwanza kulia) akimkabithi
Mhasibu wa wizara ya fedha na Mipango Fungu.
NA Mwandishi Wetu,
WIZARA ya Fedha na Mipango Fungu
Hamsini (Vote 50) linalohusika na masuala ya utawala, limeibuka kinara kwa
kupata tuzo ya mshindi wa kwanza katika utoaji wa Taarifa bora ya fedha kwa
mwaka 2016 katika kundi la Wizara na Idara za Serikali inayoandaliwa na Bodi ya
Uhasibu na Ukaguzi wa Hesabu (NBAA).
Tuzo hizo zimetolewa kwa washindi na
Mhasibu Mkuu wa Serikali, CPA. Francis Mwakapalila kwa niaba ya Katibu Mkuu wa
Wizara ya Fedha na Mipango Bw. Doto James katika Kituo cha Uhasibu na Ukaguzi
wa Hesabu kilichopo Bunju, nje kidogo ya Jiji la Dar es Salaam baada ya
kumalizika kwa Mkutano wa mwaka wa Wahasibu nchini uliofanyika katika eneo
hilo.
CPA. Mwakapalila alisema kuwa
taarifa bora za fedha ni muhimu sana katika maendeleo ya nchi kwa kuwa walipa
kodi, wawekezaji na wadau wengine hutegemea taarifa hizo katika kufanya
maamuzi.
‘Kama taarifa za fedha hazitatolewa kwa ubora unaotakiwa na kwa wakati mwafaka kunaweza kusababisha athari katika uthabiti wa mifumo ya kifedha nchini’, alieleza CPA. Mwakapalila
Aidha Mwakapalila amewapongeza
wahasibu kwa kuamua kukaa pamoja na kujadili taaluma ya uhasibu katika
maendeleo ya viwanda ambayo ni ajenda ya kipaumbele kwa Serikali ya awamu ya
tano.
Amesema suala la Uchumi wa viwanda
ni muhimu katika kuongeza kipato na kupata fedha za kigeni kwa njia ya kuuza
bidhaa nje na pia kupata mapato ya kodi na yasiyo ya kodi hivyo akatoa rai kwa
wananchi kuendelea kujadili masuala ya uchumi wa viwanda na kupata namna sahihi
ya kuufikia ili ndoto ya uchumi huo ziweze kuwa za kweli.
Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji
wa Bodi ya Uhasibu na Ukaguzi wa Hesabu (NBAA), CPA. Pius Maneno amesema kuwa
tuzo zinazotolewa na NBAA zinalengo la kuhamasisha uwajibikaji na kuandaa
taarifa ya fedha zilizo na viwango vya kimataifa.
Amesema kuwa washindi wa tuzo hizo
wanapatikana kupitia mchakato uliosheheni weledi wa hali ya juu kutoka kwa
wabobezi wa taaluma ya uhasibu nchini ambao wanaangalia vigezo kadhaa vikiwemo
kuwa na hati safi na kuwasilisha Hesabu kwa wakati na pia kufikisha kiwango cha
ubora wa taarifa kuanzia asilimia 75.
Mhasibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na
Mipango Fungu 50, Bw. Christopher Nkupama, amesema kuwa tuzo hiyo inawapa
morali ya kufanyakazi kwa umahili zaidi na kuwapongeza watumishi walioko katika
idara yake kwa kufanyakazi kubwa na bila kuchoka kuhakikisha kuwa wanazingatia
kanuni na taratibu za uhasibu wanapotekeleza majukumu yao.
Mshindi wa Jumla katika tuzo hizo
kwa taarifa bora ya fedha kwa mwaka 2016 ni Twiga Cement Plc na kwa upande wa
Wizara na Idara za Serikali ni Wizara ya Fedha na Mipango fungu hamsini (V.
50), tuzo ambayo ilipokelewa na Mhasibu Mkuu wa fungu hilo Bw. Christopher
Nkupama, ikifuatiwa na Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji fungu arobaini
na nne (V.44) na Ofisi ya Waziri Mkuu fungu ishirini na tano (V. 25)
Washiriki wa Tuzo hizo ni Mamlaka ya
Serikali za Mitaa, Wakala wa Serikali, Wizara na Idara za Serikali na Sekta
Binafsi ambapo kwa mwaka huu waliojitokeza kutoka Mamlaka ya Serikali za Mitaa
walikua sita na Wizara na Idara za Serikali walikua sita.
Jumla ya washidani waliojitokeza ni
56 na waliofanikiwa kuvuka kigezo cha kuwa na zaidi ya asilimia 75 walikua
washidi 36 na hao walifanikiwa kushika nafasi ya kwanza hadi ya tatu kulingana
na makundi.
Vilevile Idadi ya Wahasibu ambao
wamehudhuria katika Mkutano wa mwaka ambao hufanyika kila mwaka kabla ya
kutolewa tuzo hizo imepanda kwa asilimia 60 ambapo mwaka 2016 walihudhuria wajumbe 1700 ilihali mwaka huu 2017
wamehudhuria zaidi ya wajumbe 2700.
No comments:
Post a Comment